Monday, February 25, 2013

Kulemaa viungo hakuzuii akili kufanya kazi: YOHANA MAGAYI

6 comments


YOHANA MAGAYI
Naishi katika wilaya ya Bunda mkoa wa Mara, nina mke na watoto.

Kazi yangu ni ufundi seremala fani niliyoipata katika chuo cha walemavu Yombo Dar es salaam mwaka 1985  - 1986 na pia Milongo Mwanza 1988 – 1989. Pamoja na hayo nilipata mafunzo ya utetezi wa haki za binaadamu kwa watu wenye ulemavu kutoka ICD, kwahyo mimi ni mwanaharakati pia.
Kwa mujibu wa maelezo ya wazazi wangu, nililemaa baada yakuwa nimeanza kutembea nikiwa na umri wa miaka miwili (2). Niliugua polio iliyonipelekea kukaa kwa muda mrefu na baadae kunisababishia ulemavu kwa ujumla.
Nilipata changamoto kubwa katika kuliendea swala zima la kuoa, hata yule niliyekua natarajia kumuoa kabla alishtuka kusikia kua mimi mlemavu nataka kumuoa! Alifikiri kua tutazaa watoto wenye ulemavu pia. Baada ya mimi kupata mtoto wa kwanza mwaka 1988, aliniandikia barua kwamba sasa niko tayari kuolewa na wewe kwakua sikutegemea kama ungekuja kuzaa watoto wazima. Namshukuru sana mke wangu wa sasa kwa uvumilivu tangu 1988 mpaka leo.
Swala la kuoa au kuolewa nichangamoto sana kwa watu wenye ulemavu wapo wengi wanaotamani kupata wenzi wao lakini inashindikana sababu ya ulemavu walionao. Wengine wanapata wenzi lakini jamii zao zinaendelea kulalamika kwa kuona mtu asiyekua mlemavu akiolewa na mlemavu.
Kuna vikwazo vingi katika kupambana na maisha, kwa ujumla mimi ni Mwenyekiti wa kijiji na niligombea na watu wazima wenye viungo vyao vyote, jamii ilinielewa na kunichagua kuwaongoza. Lakini bado napambana na vikwazo vingi kwasababu kuna watu wanajitokeza na kuuliza maswali: ‘Hivi watu wa jamii hii hawana akili kabisa, inawezekanaje watu zaidi ya 5000 mkakubali kuongozwa na mlemavu, hamuoni kwamba huu ni udhaifu mkubwa?’. Wakati mwingine swala la kupata kipato kwa mtu mwenye ulemavu imekua ni changamoto sana. Kwa mfano sisi tunaoishi katika mkoa wa Mara ambapo shughulikubwa ya kipato ni kilimo, kitu ambacho kwa udhaifu wetu hatuwezi. Shughuli ya pili ni Uvuvi ambayo pia ni ngumu kwetu, kwahyo unakuta kupata kipato ni ngumu sana. Nashukuru kwa kazi yangu hii ya Useremala japokua ni ngumu lakini natenda na ninapata mahitaji. Nayashukuru pia mashirika haya ya ICD na mashirika mengine ambayo tunapokutana yanatupa changamoto za namna ya kujitegemea kuliko kutegemea misaada.
Mwanzoni kabisa nilikua na fikra ya ufundi toka mwanzo na ilikua ya jadi kwasababu hata baba zangu walikua wachongaji. Baadae baada ya kuingia shule nilitamani sana kua mhasibu, lakini ndoto hiyo haikufika baada ya kukosa mtu wakuniendeleza katika masomo pamoja na uwezo mkubwa niliokuanao darasani. Kwakweli mzee wangu alipata udhaifu wa kifikra, aligoma kabisa na kusema kwamba wewe hata nikikusomesha hutoweza kwenda kokote. Namlaumu sana kaka yangu ambaye alikua Dar es salaam wakati huo. Nilimwomba anitafutie nafasi ya kurudia mitihani lakini hakuweza kutekeleza hilo. Nilipokwenda Yombo nilitegemea ningepata nafasi ya kusomea uhasibu lakini baada ya kuikosa nikaamua kujiingiza kwenye ufundi kama ndoto yangu ya kwanza ilivokua. Nashukuru kwamba leo hii inanisaidia sana kwakweli. Imenitunza na kunipa mafanikio makubwa, mpaka sasa nina watoto saba (7) na watatu kati yao wamefikia elimu ya sekondari na ninasomesha wengine hakuna mtoto ambaye amenishinda. Nimefikia malengo yangu kwakweli maana namtunza mke wangu nawatunza watoto wangu pia na sijawahi kumpa mtu kunilelea mtoto hata mmoja kati ya hao saba wote.
Naishukuru sana jamii ya kijiji ninamo ishi, mpaka kufikia kunipa hadhi yakuwa mwenyekiti wa kijiji ni jambo la kushukuru sana kwakweli, inamtizamo wa pekee kabisa, kitu ambacho hata Rais hana mtizamo huo. Naishauri jamii kwa ujumla kuwaamini na kuwaheshimu watu wenye ulemavu, kilicholemaa ni baadhi ya viuongo tu, kitu kinachofanya kazi kumudu maisha ya mtu hasa ni akili, kwahyo tunaweza tukiwezeshwa. Jamii itambue kwamba sisi ni moja kati ya jamii inayofanana nao.
Naishauri serikali kupunguza ule udumavu ilionao. Kwa mfano; kuna sheria ya watu wenye ulemavu lakini wameidumaza tu tangu ilipo pitishwa mwaka 2010 mpaka leo haijatungiwa kanuni. Mpaka tunaelekea katika katiba mpya bado sheria ile haifanyi kazi na bado sina imani kama itafanyakazi. Naishauri serikali ihakikishe sheria ile inapata kanuni na kufanya kazi. Pia walemavu wapatiwe nafasi za kujiendeleza. Nashauri pia serikali ivifungue na kuviendeleza vyuo vya watu wenye ulemavu. Kwa mfano chuo cha Milongo Mwanza kimefungwa kasababu ya kukosa walimu wakati serikali ina bajeti.
Nayashauri mashirika yasiyokua ya kiserikali kama ICD, CCBRTna mengine mengi kuongeza juhudi sababu ndio yaliyosababisha watu wenye ulemavu kutambua haki zao. Nayashauri yaendelee kupiga kelele kwakuwa ndiyo yaliyotupatia mwanga, kwakuwa serikali imeweka kabatini sheria na taratibu zote za kumpatia mtu mwenye ulemavu huduma na haki zake.
Read More ->>

Monday, February 18, 2013

HAKI ZA BINADAMU NA ULEMAVU KIKATIBA

0 comments


HAKI ZA BINADAMU NA ULEMAVU KIKATIBA


KUTANZUA ULEMAVU KUPITIA MCHAKATO WA KATIBA YA ZAMANI NA KUINGIZA KATIKA KATIBA MPYA YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA


KUTANZUA ULEMAVU KUPITIA MCHAKATO WA KATIBA YA ZAMANI NA KUINGIZA KATIKA KATIBA (SOLUTIONS  ON  DISABILITY BARRIERS)
HAKI ZA BINADAMU KWA WATU WENYE ULEMAVU KIKATIBA
Utangulizi
Kwa muda mrefu sasa watu wenye ulemavu (wwu)  nchini wamekuwa wakinyanyaswa na kunyimwa haki zao za ajira, elimu, afya na utengamao wa maisha yao. Mfumo wa sheria umechelewa sana kwani baada ya miaka 50 tangu kupata uhuru watu wenye ulemavu ndiyo wamefanikiwa kushawishi kutungwa kwa sheria namba 9 ya 2010 inayohusu Haki na ulinzi kwa watu wenye ulemavu (WWU)Tanzania.

Haki za watu wenye ulemavu zinatokana na msingi wa kikatiba kama ilivyo makundi mengine katika jamii. Kipengele cha Haki ya usawa, Ibara ya 13 ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inakataza aina zote za ubaguzi, yaani ubaguzi wa rangi, utaifa, Jinsia,  na hali nyinginezo yaani ikiwemo na kundi la watu wenye ulemavu.

Pia matamko mbalimbali ya Umoja wa mataifa yatambua kuwepo kwa kundi hili la ,hasusani watu wenye ulemavu.Tamko la Haki za binadamu la mwaka 1948, na kanuni za fursa sawa na haki kwa WWU za Umoja wa Mataifa na mkataba wa kimataifa wa ulinzi wa haki na hadhi kwa WWU  tamko hili linajulikana kama ‘’ Mkataba wa kimataifa wa kulinda Haki na Hadhi za watu wenye ulemavu’’. Na mnamo tarehe 24.04.2009 bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania liridhia mkataba huo, kitendo ambacho kimesababisha mkataba huu kutumika nchini kama mojawapo ya nyenzo ya kutungwa  kwa Sheria namba 9 ya mwaka 2010 inayohusu Haki na ulinzi kwa watu wenye ulemavu Tanzania.

Falsafa ya Ulemavu
Kihistoria watu wenye ulemavu kwa muda mrefu sana wamekumbwa na vikwazo vya aina nyingi, na kikubwa kuliko yote ni ile hali ya unyanyapaa.katika jamii za kale kila mwanajamii alikuwa na wajibu  wa kutoa mchango fulani katika uzalishaji mali na utafutaji chakula.
Mtu anapotokea kupoteza moja ya viungo vyake, ni wazi kwamba atashindwa kushiriki  kikamilifu  katika harakati za uzalishaji mali hasa kipindi hicho cha kale ambapo sayansi na tenkolojia ilikuwa duni  hivyo basi matokeo yake tamaduni zetu za kiafrika  zinaufananisha ulemavu na mambo kama vile adhabu, laana, mkosi ndio maana baadhi ya makabila yaliwaua , kuwatupa kuwatekeleza na kuwaficha majumbani mwao kwa kuhofia aibu.
Huu ndio msingi mkubwa unaosababisha hata watunga sera  zetu wakawa na mtazamo wa namna hii. Wataalamu wa mambo ya watu wenye ulemavu wanawagawa makundi ya jamii sehemu tatu kama ifuatavyo;
Kundi  la kwanza: Mbinu ya makundi ya hisani;
Ni yale tu ambayo yanamshughulikia au kumsaidia mtu mwenye ulemavu kwa sababu ya hofu ya Mungu na siyo kwa kujali utu wa huyo mhusika, kutoa vihela vichache, chakula, tafrija, wakiamini kwamba watapata thawabu kwa muumba wao.

Kundi la pili:  Mbinu /mtazamo wa tiba;
Ni watu ambao wanaona kwamba mtu mwenye ulemavu ni sawa na mgonjwa anayehitaji kutibiwa, hivyo basi hufanya harakati nyingi ili kuhakikisha kwamba, hali ya mtu mwenye ulemavu inakuwa bora kwa kumkarabati na kujaribu kumrudisha katika hali yake ya awali.
Kundi hili ni la hatari pia kwa sababu wakati mwingine limekuwa likibuni mbinu za kisayansi kama vile kuharibu mimba ambayo wanadhani kwamba mtoto atakayezaliwa atakuwa mtoto ni mtoto mwenye ulemavu au kumwangamiza mara tu atakapozaliwa na ulemavu hasa wakifahamu kwamba hawezi kufanyiwa ukarabati wa aina yoyote.
 Kwa upande wa Viziwi kundi hili linakarabati masikio kwa kuweka vitu mbadala ili kulazimisha Kiziwi asikie kwa kutumia vifaa hivyo (Cholera Implant).
 Kwa kufanya hivyo kuna matokeo zaidi ya kuwa Kiziwi, kwani katika kukarabati wakati mwingine Kiziwi anapooza au kupinda kwa baadhi ya viungo kama vile mdomo, taya, na macho. Anakuwa Kiziwi na kuongezewa ulemavu mwingine.
Kundi la pili:  Mbinu /mtazamo wa Kijamii;
Kundi hili ni lililohamasika. Hili hutanguliza utu wa mhusika kabla ya kufikiria udhaifu wake. Lengo la kundi hili ni kuvitumia vipaji vingine alivyo navyo MMU na kumpa elimu, nyenzo na mbinu mbalimbali na kumwezesha mtu huyo kuchangamanika na jamii na kujiletea maisha bora kama wanajamii wengine. Kundi hili ndilo linaungwa mkono na wanaharakati wa WWU duniani kote.
KUTANZUA VIKWAZO KWA  WATU WENYE ULEMAVU NCHINI TANZANIA
Vikwazo kwa watu wenye ulemavu Duniani vinafanana na ni vingi, lakini wanaharakati wa haki za watu wenye ulemavu (WWU) wanavigawa katika makundi matatu kama ifuatavyo;
Kikwazo cha Kimtazamo hasi/Attitudinal
Huu ni ubaguzi wa kijamii kwa WWU kwa kutafsiri  au kuangalia  ulemavu katika hali hasi, ni balaa, mkosi laana na aibu. Hili linawakuta wote, WWU na jamii. Ni suala la ujinga kuhusu visababishi vya ulemavu na kukata tamaa juu ya kile wanachomudu kufanya au kutelekeleza WWU katika jamii mfano;
1.    Tumeamua kuwa huwezi/Je, unataka sisi tukulipie matibabu “ Hongera sana”  (We have decided you can not, Do you want us to pay for your treatment, ‘’Very brave’’)

2.    Sawa,  sihitaji msaada…, Maskini mwanangu – (Its ok I don’t need help, Poor child)

3.    Ni bora ufanye kazi mahali penye kelele, Haitakudhuru kitu… (Good to work in noisy place, Can not expect to…)
Je, tufanyeje? Katiba ya Tanzania itanzue kikwazo hiki kwa kutamka kwamba…
  1. Serikali  na Taasisi zake za umma kwa ujumla vinatoa haki na nafasi zilizo sawa kwa raia wote, wake kwa waume, bila ya kujali rangi, kabila, dini au hali ya mtu kuwa na ulemavu.
  2. Hautakuwepo ubaguzi wa aina yoyote, ujinga au uoga wa aina yoyote katika Sekta za umma, sekta binafsi, Taasisi za  kimaendeleo , Jamii na familia katika kutoa kipaumbele kwa kuwajumuisha wwu katika utekelezaji wa mipango inayopangwa na kuendeleza vipaji walivyo navyo wwu kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Kikwazo cha Kimazingira/ The barrier of Environmental
Ni ubaguzi wa hali ya kuwatenga watu wenye ulemavu pale majengo ya umma au yale yatoayo huduma kwa umma, vyombo vya usafiri, bidhaa na huduma mbalimbali, vinaposanifiwa, kujengwa au kutolewa bila kutilia maanani mahitaji maalum ya WWU, mathalani wale wenye tatizo la ujongeaji, mfano;
1.    Maji/ Visima/ bomba- Water/well/Tap, Public buildings,Washrooms, Homes

2.    Michezo/Burudani/mawasiliano na shule/ Sports/Leisure, Communications, School

3.    Vigumu kupanda cheo,Vituao vya afya, na usafiri/ Difficult for promotion, Health centers,Transport etc.

Je, tufanyeje? Katiba ya Tanzania itanzue kikwazo hiki kwa kutamka kwamba…
1.    Miundo mbinu yote ya umma, mfano majengo, vyombo vya usafiri, barabara, njia, iwe vinafikika, vinaendeshwa  na inatumika bila kikwazo kwa kila mtu na kwa wakati wote.

2.    Lugha za Taifa za  Mawasiliano ni Kiswahili, Kiingereza, Lugha ya alama (katika kuwasiliana na wenye ulemavu kiziwi), Maandishi ya nukta nundu (katika kuwasiliana wenye ulemavu wa kutoona) Kila sehemu inayotumika na umma kuwepo na uwezeshaji wa lugha hizi kikamilifu.
Kikwazo cha kisera na kisheria/Institutional
Ubaguzi huu umekuwa ikitokea duniani kwa kudhamiria au kutodhamiria hadi miaka ya hivi karibuni. Ndiyo maana kuna makundi ya raia yanayoitwa ya pembezoni miongoni mwao wakiwemo WWU. Kubaguliwa huku kumechangiwa sana na makundi husika kutokuwa na sauti ya pamoja katika uhamasishaji, uraghibishi na utetezi.

Kulihibuka na wanaharakati wenye fikra za kimapinduzi za kitafiti na kugundua na kutegua kitendawili cha ulemavu kwa kutofautisha na neno ki/vilema. Na kuwa ‘’Kilema chake siyo tatizo, bali jamii iliyomzunguka’’

Ubaguzi huu unatokea pale sheria, kanuni au miongozo, sera au mipango ya maendeleo inaposhindwa kutaja bayana ni kwa jinsi gani watu wenye ulemavu watanufaika.  Ukimya huu, huwafanya wahusika ndani ya kundi hili kwa namna moja au nyingine waonekane raia daraja la pili wasio na haki ya kupata fursa ya kujiendeleza kihali na kiakili kama vile kupata elimu, kuajiriwa, masuala ya siasa, kujiwakilisha kwenye vyombo ya utungaji sera, kufanya maamuzi ngazi mbali mbali na kuzaa na kulea watoto nk. Mfano;
1.    Imani potofu, haiwezekani kugombea au kupiga kura au kuwakilishwa, wakilisha –
( Tradition, Can not stand for election or representation, No vote).

2.    Hakuna kufunga ndoa, ajira, hakuna haki ya kuwa na ardhi- ( No marriage,employment, No land rights)
3.    Masuala ya uchumi, mfano benki mikopo au mikataba- (Bank/credit/Loan, formal contracts)

Je, tufanyeje? Katiba ya Tanzania itanzue kikwazo hiki kwa kutamka kwamba…
1.    Mamlaka mahsusi ya nchi au Baraza kama ilivyotajwa katika sheria ya mwaka 2010 ya itawekwa chini ya ofisi ya  Ofisi ya Rais au Makamu  wa Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania ili kuratibu kimantiki na kuhakikisha kwamba sera ya mwaka 2004 inaboreshwa zaidi, inakidhi makundi tofauti tofauti ya watu wenye ulemavu na vyama vyote vilivyosajiriwa kihalali kisheria katika mamlaka zote za usajili kuanzia ngazi ya Taifa, vinajumuishwa katika mamlaka hiyo. Vile ile kila Wizara na taasisi zake zitakuwa na dawati linaloshughulikia masuala ya wwu.

2.    Mamlaka mahsusi ya nchi au Baraza kama ilivyotajwa katika sheria ya mwaka 2010 inaratibu kimantiki na kuhakikisha kwamba Mkataba wa kimataifa wa kulinda Haki na Hadhi za watu wenye ulemavu’’ Na Sheria namba 9 ya mwaka 2010 inayohusu Haki na ulinzi kwa watu wenye ulemavu Tanzania inatekelezwa kwa kufuata wakati na kutoa mrejesho unaotakiwa kikamilifu.

1.    Watu wenye ulemavu wawe na nafasi maalum za uwakilishi, kulingana na uanisho la makundi  ya ulemavu kama vile wenye ulemavu  wa viungo, wasioona, Albino, Viziwi, Viziwiwasioona, Uti wa mgongo, Akili, Kupooza, na ulemavu mwingine mchanganyiko, pia kutakuwepo na wagombea wwu binafsi walio na uwezo kutumikia nchi wanaogombea uongozi wa kisiasa miongoni wa makundi ya watu wenye ulemavu ili kuingia katika vikao vya maamuzi ambavyo ni Bunge, Halmashauri/Manispaa, Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji.

2.     Kila panapotokea Rais, Waziri au mkuu yoyote wa kisiasa, Mtunga sera, na mtoa maamuzi anakuwa na  fursa ya kuteua mtanzania kufanya kazi za umma, atawasiliana na Mamlaka mahsusi iliyowekwa  ili kuona uwezekano wa kuteua pia mtu mwenye ulemavu.
3.    Watu wenye ulemavu watafaidika na rasilimali za nchi  kutoka Serikalini katika ngazi zote (Serikali kuu na Halmashauri/Jiji/Manipaaa) itatoa ruzuku asilimia 10% ya mapato kwa vyama vya watu wenye ulemavu ili viweze kuendesha shughuli zao kimaendeleo  na kupunguza utegemezi katika jamii. Vigezo kuzingatiwa chini ya mamlaka husika.

4.    Huduma zote za umma itakuwa ni bure kwa watu wenye ulemavu, serikali itawajibika kugharamia huduma zote kwa asilimia 100%.
5.     Kupitia mamlaka husika, Serikali itawezesha tafiti kwa wingi na za kutosha zinazohusu watu wenye ulemavu ili waweze kupanga maendeleo yao kwa uhakika, kuwa  na taarifa za madai ya kueleweka, wasionekane  kama watu wa kulalamika tu  na wasio  na hoja za msingi. Hii ni sehemu mojawapo ya wajibu.
Tafakari!!
1.     Hakuna chochote kuhusu sisi bila sisi kushirikishwa!!!!!!

2.     ‘’Tusisubiri maamuzi yafanywe wengine kwa niaba yetu kisha tunaanza kulalamika kuhusiana na maamuzi hayo’’ ( Mwl JK. Nyerere)

Read More ->>

Sunday, February 17, 2013

Vishawishi vya wanajamii vilimfanya mume wangu anikimbie: PELESIANA JULIUS

0 comments


Naitwa Pelesiana Julius natokea mji wa Bunda naishi katika mtaa wa mbugani. Nina umri wa miaka 36 na nina ulemavu wa viungo (natembea kwa kutambaa).

Mimi nilizaliwa nikiwa mzima na tulikua mapacha wawili, baadae mwenzangu akaugua na kufariki. Baada ya Kurwa kufariki basi ungonjwa ukawa umenishika mimi, niliugua kwa muda mrefu sana, mama angu akanizungusha mahosipitalini na kwa waganga mbalimbali matokeo yake miguu ikawa imepooza na ndo chanzo cha kupata ulemavu huu.
Kwasasahivi sina mume lakini kwa kipindi cha nyuma nilikua na mume aliye nizalisha watoto watatu (3), baadae akawa ameshawishika kwamba utaishije na mtu kiwete huwezi kutokanae hata matembezi? Akawa amekubaliana na hivyo vishawishi na kuondoka mwaka 2004 na kuniacha nahangaika na watoto. Namshukuru Mungu kwasasa wanangu wameishakua watu wazima na wanaweza kujihangaikia.
Maisha yanakua magumu kulingana na hali na shughuli ninazozifanya pia, unakuta shughuli zinakwama zinakua ngumu na watoto unao,pakukimbilia unakua huna. Hata ukikimbilia kwa ndugu, ni ndugu wachache wanaoweza kukusaidia, kila mtu atasema anaangalia mambo yake. Kwakweli nakua na shida nyingi sana nahangaika, hata sehemu za kuishi unaishi kwa shidashida. Nashukuru Mungu alinisaidia nikawa nimejenga kinyumba kidogo cha tope, lakini pia bado ninahangaika kwasababu nilipata kiwanja maeneo ya majimaji. Mvua zinapokuja nyingi zinanipa shida sana nahangaika, pamoja na hayo sina msaada wowote kusema mtu anaweza akanisaidia hata kwa kuniletea gari moja ya mawe ili ninyanyue nyumba iwe juu.
Naishauri serikali kwakweli itusaidie watu wenye ulemavu maan tunapata shida sana hasa swala la makazi na mazingira. Unaweza mtu ukawa unaishi nyumbani lakini unakuta choo kichafu, bafu chafu sasa jinsi ya kufanya usafi kwa mtu mwenye ulemavu inakua ni ngumu sana. Naiomba serikali itukumbuke sisi watu wenye ulemavu hata kama wale ambao Mungu ametusaidia tumepata sehemu za kujenga nyumba zetu wenyewe, serikali itusaidie hata kutuwezesha kujenga nyumba nzuri zenye vyoo vizuri vya kufikika ili nasisi tufurahie maisha.
Jamii naishauri imuangalie mtu mwenye ulemavu kama binaadamu wa kawaida kwasababu sehemu zingine tunaonekana kama watu wasio faa, inatakiwe watupe haki sawa kama watu wazima. Jamii isitunyanyase sababu ya ulemavu wetu. Walemavu wengi sana unakuta wametengwa sana. Unakuta mtu ni mchafumchafu tu. Sasa ule uchafu unakuta unatokana na kukosa msaada lakini sio kwamba jamii haiwezi kumsaidia ila wanaona kwakua ni mlemavu hana manufaa kwao. Tunahitaji jamii ituangalie kuwa nasisi ni watu.
Kwaupande wangu sipendi sana kulalamika, napia namshukuru Mungu kwasababu sipendi kukaa kwasababu eti ni mlemavu maana kama ni kulemaa nimelemaa miguu ila sijalemaa akili. Kwahyo ninacho washauri walemavu wenzangu nikwamba, kama mtu unao ulemavu unaokuruhusu kujishughulisha basi jishughulishe. Usije ukajiweka kwamba wewe ni mlemavu ukategemea jamii au serikali ikusaidie, kwa upande mwingine inakua ngumu. Pamoja nakwamba tunahitaji misaada kama watu wenye ulemavu lakini na sisi tunatakiwa tujipe nguvu ya kuweza kujisaidia wenyewe. Kwasababu mtu hata atakapokuona wewe unakua na kazi ya kufanya inayo weza kukupa kipato kidogo, unaweza ukakimbilia kwa mtu mwingine akakusaidia kulingana na kazi unayoifanya. Sasa ukiwa umekaa tu huwezi kukimbilia kwa mtu akukopeshe hata elfu tano (5000) akakubari sababu anajua huwezi kuipata kwa kukaa tu, lakini ukiwa unajishughulisha kama mlemavu unaweza kwenda sehemu ukakopa pesa pamoja nakwamba biashara kwetu zinakua ngumu kutokana na ufikikaji wa maeneo au kukosa msaada lakini inatubidi tushughulike kama watu wenye ulemavu. Serikali ijitahidi kutukumbuka jamani.
Read More ->>
 

| DISABILITY IN TANZANIA INFORMATION PLATFORM © 2012. All Rights Reserved |Designed by MIRAMBO GROUP | Back To Top |