Sunday, January 20, 2013

MKASA WA MLEMAVU ANAYETESEKA BADA YA KUBAKWA

0 comments



Asha Musa (katikati) akiwa na bibiu yakew na mtoto wake.

SIKU hizi kuna watu wanasema; “Ni heri ukutane na mnyama mkali kama, simba au chui unaweza kusalimika, kuliko kukutana na binadamu, kwani anaweza kukudhuru.”
Maneno haya yanatokana na unyama wanaofanyiana  wenyewe kwa wenyewe.

Kila siku tunasikia unyama unaofanywa na binadamu, leo utasikia baba wa miaka 45 amemnajisi mtoto wa miezi minne, mke amemkata na shoka hawara wa mume wake, majambazi wameua familia nzima na mambo kama hayo.
Hayo yanadhihirishwa na mkasa  wa Aisha (siyo jina lake halisi), aliye na  ulemavu,  ambaye hajiwezi kwa lolote bila msaada wa mtu.

Hata hivyo, pamoja na hali aliyonayo, bila chembe ya huruma, Aisha amekuwa mwathirika wa unyama wa binadamu, baada ya kubakwa.
Binti huyo anaishi katika Kijiji cha Ntisi, Kata ya Bicha, umbali wa kilometa tano kutoka Kondoa Mjini, eneo ambalo hakuna usafiri mwingine unaoweza kukufikisha zaidi ya bodaboda.
Katika kijiji hicho hakuna asiyemfahamu binti huyo kutokana na hali yake na historia ya maisha yake, ambayo inasikitisha kila aliye karibu naye.

Kwa takriban miaka 21, binti huyo ameishi na bibi yake aitwaye Mwajabu Haji, lakini sasa familia hiyo imeongezeka, baada ya Aisha kujifungua mtoto, ambaye ni zao la kubakwa. Mtoto huyo sasa ana umri wa miaka sita.
Ukifika nyumbani kwao utamkuta Aisha amekaa katika kiti chake maalumu cha mbao, alichotengenezewa na bibi yake.
Hana kiungo chochote mwilini mwake kinachoweza kufanya kazi zaidi ya mdomo wake.

Hata hivyo, inzi humwingia mdomoni na kutoka, wakirukaruka katika mwili wake wapendavyo, kwani binti huyo hawezi kuwafukuza kwa kuwa mikono yake haifanyi kazi.
Umbile lake lilivyo
Zaidi ya kuzungumza, Aisha hawezi kufanya shughuli yoyote kutokana na kuwa, mikono na miguu vimejipindapinda.

Tumbo lake limesogea upande wa kushoto na kichwa  kulia.
Mara nyingi anapoongea mikono hupata nguvu ya ajabu ambapo huanza kurukaruka huku na kule kwa kuwa hawezi kuizuia, hujigonga na kujiumiza katika sehemu mbalimbali.

Mikono hiyo haina nguvu ya kuweza kubeba kitu chochote  au kufukuza wadudu wanaotambaa katika mwili wake hasa inzi kutokana na vidonda vilivyojaa.
Historia ya maisha yake
Aisha  alizaliwa mwaka 1990 Musoma, mkoani Mara akiwa na ulemavu. Alipofikisha umri wa mwaka mmoja, alipelekwa kwa bibi yake mzaa mama, baada ya baba yake kukataa kuendelea kumlea. “Kwa kweli ninamshukuru Mungu na bibi yangu kwa kiasi kikubwa,  kwa kuwa katika historia yangu, nimekutana na changamoto nyingi, lakini hakunitupa au kuninyanyapaa,” anasema na kuongeza:
“Ninamhurumia bibi kwa kuwa pamoja uzee, lakini hana budi kubeba, jukumu la kututafutia riziki ya kila siku kwa ajili yangu na mtoto wangu.

Natamani ningekuwa na uwezo hata wa kumsaidia kuosha vyombo,” anasema Aisha.

Anasimulia kuwa, kwa mujibu wa bibi yake, mama yake alilazimika kumrudisha kijijini hapo, baada ya baba yake kutaka wamchinje au wamtupe.
Aisha anaeleza kwamba, kwa kuwa mama yake alikuwa akiipenda ndoa yake, hakuwa tayari kumtupa au kumuua badala yake alimpeleka kwa bibi yake, ili kuokoa uhai wake.
“Mama yangu mzazi aliwahi kupigwa na baba,  huku akitishiwa kuachwa endapo atanilea, ndugu zake baba walimshauri anitupe,” anasema Aisha.

Anaongeza kuwa, hajawahi kukutana na baba yake mzazi, lakini anadai kuwa anamfahamu kwa jina la David Chacha akieleza kuwa anafanya kazi ya upishi jeshini huko Monduli.

Mama yake mzazi ambaye pamoja na kumrudisha kwa bibi yake, alikuwa akifika kijijini hapo mara kwa mara kumjulia hali, hata hivyo alifariki mwaka 2011.
Alivyobakwa mpaka kupata ujauzito
Kutokana na umbile lake lilivyo na pilikapilika za bibi wa Aisha katika kutafuta riziki, ilimchukua miezi saba bibi huyo kugundua kuwa mjukuu wake ana ujauzito.

Bibi huyo anasema kuwa aligundua kuwa mjukuu wake ana ujauzito, wakati tayari imeshafikisha miezi saba.

Anaeleza kuwa alibaini kuwa matiti ya Aisha yakiwa yamejaa, ndipo alipomchunguza vizuri na kugundua kuwa ni mjamzito.
Mwajabu (Bibi wa Aisha) anasimulia kuwa alipomuuliza Aisha kutaka kujua aliyempa ujauzito na jinsi alivyoupata, alishangaa kwa kuwa, aliyempa ujauzito huo ni binadamu mwenye akili timamu.
Anasema kuwa baada ya hapo alimpeleka mjukuu wake kliniki, lakini pia alimtafuta kijana aliyempa ujauzito, ambaye anafahamika kwa jina moja la Mashoto.
“Bibi mimi huingiliwa na mwanamume  aitwaye Mashoto, ila kaniambia nisimtaje, ikitokea nimemtaja basi atanichinja ndiyo maana nilinyamaza, nikiogopa kuchinjwa,” anaeleza Mwajabu akimnukuu Aisha alipotaka kujua aliyempa ujauzito.

Baadaye, bibi huyo aliamua kwenda polisi kutoa taarifa, ambapo aliambiwa atoe Sh500, ili mgambo watumwe kwenda kumkamata Mashoto.
Mgambo hao walifanikiwa kumtia ndani mtuhumiwa,  lakini baada ya siku chache alitoka na kuwaomba waifute kesi kwa madai kuwa atamtunza binti huyo na mtoto atakayezaliwa.

“Sijawahi kupata msaada wowote kutoka kwa mwanamume huyo tangu wakati huo, mpaka sasa mjukuu wangu ametimiza miaka sita, lakini nimeamua kumuachia Mungu,” anasema Mwajabu.
Akisimulia kuhusu ujauzito wake, Aisha anasema kuwa alipitia wakati mgumu, kwani hakuwa na msaada wa kupata mahitaji muhimu.

Anasema kuwa mtu pekee aliyemfanyia wema mbali na bibi yake ni daktari aliyemhudumia wakati akijifungua, akisema kwamba kamwe hawezi kumsahau.
“Sikutaka kupoteza kumbukumbu ya daktari yule, Novatus Kasongo, nikaamua kumpa jina hilo mtoto wangu, alikuwa mwema na alinisaidia,” anasema Aisha.
Msaada anaohitaji
Hatima ya familia hiyo ipo chini ya bibi Mwajabu ambaye hana shughuli nyingine anayoweza kufanya zaidi ya kilimo cha jembe la mkono. Lakini pia hawezi kulima mashamba ya mbali kwa kuwa ana jukumu la kumuangalia mjukuu wake yake huyo na kumfanyia kila kitu ikiwemo kumtoa nje na kumrudisha ndani jioni.
“Ninaishi kwa kutegemea kilimo cha jembe la mkono, lakini pia siwezi kulima sana kwa kuwa nina jukumu jingine la kumwangalia mjukuu wangu na mtoto wake,” anasema na kuongeza:
Pia siwezi kwenda mbali kwa kuwa inabidi nimwangalie mjukuu wangu, ambaye hajiwezi kwa chochote, hapa nilipo ninaumwa kifua kwa sababu ya kumbeba kila siku wakati wa kumtoa nje na kumrudisha ndani jioni,” anasema.

Anaongeza: “Ninaomba wasamaria wema wanisaidie chakula, nguo na kitukuu changu kusoma, hivi sasa umri wake anatakiwa kuwa shuleni lakini sina uwezo. ninaomba wanaoguswa na hili wanihurumie.
Pia ninaomba msaada wa kiti maalumu kwa ajili ya mjukuu wangu, akiwa na kiti itanipunguzia kazi kwani nitakuwa nikimsukuma tu.”

Habari hii ni kwa Hisani ya MPEKUZI (www.freebongo.blogspot.com)
Read More ->>

Sunday, January 13, 2013

CHRISTINA MAUMA

0 comments


Naitwa Christina Mauma mkazi wa kijiji cha Kiara, nina ulemavu wa macho na sifanyi kazi.

Nina mtoto mmoja ambaye naishinaye na kumtunza. Ulamavu nilionao nilizaliwanao.
Katika maisha ya kila siku nakumbana na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na kukosa msaada wa kumpeleka mtoto shule. Miundombinu kutokua rafiki na ukosefu wa huduma tengamavu kwa watu wenye ulemavu.
Naishauri jamii kuwapenda na kuwathamini watu wenye ulemavu. Watu wenye ulemavu ni sawa na watu wengine wanahitilafu ndogo tu katika viungo vyao ila wanahitaji kupendwa na kuthaminiwa kama watu wengine.
Serikali ijitahidi sana kuwajali na kutekeleza mahitaji ya watu wenye ulemavu kwa vitendo isiishie kuzungumza kwenye majukwaa tu.
Walemavu wenzangu wajitahidi kua karibu na jamii na tusijiweke mbali na hata katika kazi tusaidiane kwa pamoja ili tusiendelee kuonekana kua tuko nyuma sana.
Mashirika na asasi mbalimbali wajitahidi kuzidi kuwatia moyo watu wenye ulemavu bila ubaguzi. Pia mashirika yanapokua yanaita wawakilishi wa kuwasaidia katika shughuli mbalimbali wilayani na mikoani wajitahidi kuwahusisha hata walemavu wasio wafanyakazi. Kitendo cha kuwatumia wafanyakazi pekee kwa mfano; walimu ni kuwanyima walemavu wasio na ajira fursa ya kujifunza na kutetea haki zao.
Read More ->>

Wednesday, January 9, 2013

SURUA na IMANI POTOFU vilinisababishia ULEMAVU: EDWARD JUMA MWITA

0 comments


Naitwa Edaward Juma Mwita, mkazi wa Musoma mjini mkoa wa Mara. 

Nina ulemavu wa macho (uoni) ambao sikuzaliwa nao ila tu niliugua surua nikiwa na miaka mitatu (3). Baada yakupelekwa hospitalini ikagundulika kua macho yangu yalikua yameharibika na nisingeweza kuona tena. Tatizo langu lilichangiwa kwa kiasi kikubwa na imani potofu zilizokua zimetawala kwa kipindi hicho. Baada ya kuugua surua ilisemekana kua huyu mtoto (mimi) hatakiwi kuonekana kwa watu hivyo niliwekwa ndani. Badae mama ndo alikuja kugundua kua macho yalikua yanaharibika baada ya kufungua kope za macho yangu, badae wakaamua kunipeleka hospitalini lakini walikua wameisha chelewa.
Nilibahatika kusoma mpaka elimu ya sekondari lakini sikufanikiwa kuendelea zaidi kwasababu ya gharama za masomo pamoja na ukosekanaji wa vifaa. Kwasasa naishi na mama yangu sijaoa wala sina mchumba.
Changamoto kubwa ninayo kumbananayo ni upatikanaji wa mahitaji muhimu ya kuniwezesha kuishi kama mwanaadamu wa kawaida, kwamfano; chakula, malazi na mavazi inakua vigumu sana kuvipata hasa pale unapokua huna shughuli ya kukupatia kipato.
Wakati mwingine sio rahisi sana kukubalika katika jamii. Inachukua muda mrefu kwa jamii kuja kukukubali, labda waone tu umefanya kitu flani ambacho kinawezakua ni kivutio kwao. Kwamfano; Niliwahi kumwelekeza jamaa mmoja aliyekua anatafuta duka flani hapa Musoma, nikamwambia kua twende mimi ntakupeleka lakini hakutaka kuniamini. Sasa hii ni sehemu ya changamoto ninazo kumbananazo sababu kile ambacho mi nakitenda hakiataaminika mpaka mwenye macho akithibitishe kwamba ni kweli nakiweza ama sikiwezi. Kwahyo kukubalika kwangu kutategemea uwezo wangu katika kukiweza hicho kitu. Hii inapelekea mambo mengi kua magumu kufanyika sababu sio kitu kizuri kumwambia mtu kua hiki kitu ntakufanyia halafu asiwe na imani!.
Changamoto nyingine iko katika swala la fimbo nyeupe ambazo ni chache. Pamoja na kua chache bado hazitoi ishara kukufahamisha kama kuna kitu flani mbele yako ambacho unatakiwa kua tayari kukikabiri, hii inapelekea ugumu flani katika kutembea kwa watu wasio ona. Kama kungekua na uwezekano basi tungeweza kupatiwa fimbo zenye uwezo huo ili tuweze kutembea salama na kwa uhakika.
Nilikua na ndoto zakuja kua mwanasheria au mwalimu lakini sijafanikiwa kuzifikia ndoto zangu. Pamoja na kusoma kwa changamoto nyingi sana hasa katika elimu ya msingi ambapo ilikua inakulazimu kuwategemea watu wakusomee ili uweze kuandika lakini bado nilikua na ndoto za kuendelea na nilifanya hivo. Nilianza kupata shida kubwa sana kipindi nilipoingia sekondari, ilikua inamlazimu mtu awe na pesa ili amtafute mtu umpatie fedha ili akusomee na wewe uandike. Kwasababu kinachofanyika sekondari baada ya mwalimu kufundisha na kuandika notisi huwezi kusomewa humohumo darsani kama ilivokua shule ya msingi. Inakubidi baada ya vipindi umtafute mtu mwenye macho kwa muda wako na pesa yako mwenyewe ukaenae kwenye chumba maalumu akusomee na uanze kuandika masomo ya siku nzima. Pamoja na hayo, karatasi (kwaajili ya kuandikia watu wenye ulemavu wa macho) zinakua ni duni maana upatikanaji wake ni tatizo, kunawakati zinaweza kukosekana mpaka kipindi cha mwezi mzima na kwakipindi hicho chote walimu wanaendelea kufundisha na notisi zinaongezeka pia. Kwahyo utakapoanza tena kuandika masomo tisa utakua umepoteza muda mwingi sana kiasi kwamba hata muda wakujisomea unakua hadimu pia.Hivyo inakupatia mzigo mkubwa tena wa kukisoma kitu ambacho kilisha fundishwa muda mrefu uliopita na wakati huohuo kukisoma kitu kilichofundishwa kwa wakati huo. Hali hii inasababisha walemavu hasa wasioona warudi kua ombaomba katika mitaa mbalimbali ya nchi hii.
Naiomba jamii iweze kuwathamini na kuwasaidia watu wenye ulemavu kwasababu watu wenye ulemavu hususani wasioona wanaishi katika mazingira magumu sana. Asiyeona asipokua na pato lolote anapata taabu sana. Naiomba jamii iwe tayari kuwasaidia watu wenye ulemavu, nafahamu kua kuna wenzetu ambao sio waaminifu lakini kama hao watu wakikutokea na ukafahamu mwachie Mungu tu kwakua wewe umeishatoa. Pia naiomba jamii ishiriki kikamilifu katika kuwasaidia watu ambao wako katika mazingira yanayoweza kuwapelekea kua walemavu ilikusudi waepukane na hali hii ya ulemavu kwani ni tatizo kubwa mno.
Watu wenyeulemavu wenzangu nawashauri tuendelee kujitahidi pale tunapokua tumepata nafasi mbalimbali kama shule au ajira ili tuweze kujiendeleza. Pia kile ambacho tunakipata kama misaada  inatakiwa tukitumie kwa uaminifu mkubwa ili mtu anapokuja tena kuangalia kile unachokifanya akute umefanya vizuri. Kwahyo nivyema tukafanya kazi kulingana na uwezo aliotuwezesha Mungu, tusilemae tu kwa kisingizio cha ulemavu.
Naziomba asasi mbalimbali hasa zile zinazojishughulisha na maswala ya watu wenye ulemavu zifanye kazi zake kulingana na lengo la kuanzishwa kwake, wasitumie vibaya misaada wanayopewa. Pia wajitahidi kuvumbua vitu mbalimbali vinavoweza kuwasaidia watu wenye ulemavu sio tu kuendelea kutoa habari kuhusu haki zetu.
Serikali yetu ijitahidi sana kutekeleza wajibu wake. Tunazo rasilimali nyingi sana ambazo zikitumiwa vizuri zinaweza kuwasaidia watu wenye ulemavu. Hivyo rasilimali zilenge makundi yote. Misaada itolewe kwa vyama vya watu wenye ulemavu ilikusudi hata watu wenye ulemavu waweze kukopa kupitia vyama vyao wenyewe. Pia vilevile katika zile nafasi kumi (10) za wabunge wa kuteuliwa zingetolewa nafasi kwaajili wa vyama vya watu wenye ulemavu kuteuliwa ili tuweze kupata wawakilishi katika vyombo vya kufanya maamuzi.
 Nawaomba sana ndugu zangu wasioona ambao wako mashuleni wajitahidi sana kusome kwabidii pamoja na changamoto nyingi wanazokumbana nazo.
Read More ->>

Monday, January 7, 2013

HOTUBA YA WAZIRI WA AFYA KATIKA MAADIMISHO YA SIKU YA KIMATAIFA YA MAANDISHI YA BRAILLE TAREHE 4 JANUARI, 2013

0 comments




HOTUBA YA MGENI RASMI


WAZIRI WA AFYA NA USTAWI WA JAMII


MHESHIMIWA DKT.HUSSEIN ALI MWINYI (MB)


KATIKA MAADHIMISHO YA SIKU YA KIMATAIFA YA
MAANDISHI YA BRAILLE TAREHE 4 JANUARI, 2013

·        M/kiti wa Taasisi ya Huduma na Maendeleo kwa Wasioona Tanzania
·        Ndugu Viongozi, Wadau na Wanachama wa Taasisi ya Huduma na Maendeleo kwa Wasioona,
·        Wananchi wote mliohudhuria hapa, Mabibi na Mabwana.

Kwanza kabisa napenda kuwatakia heri ya mwaka mpya 2013. Pili napenda nichukue fursa hii kuwashukuru kwa kunialika kuja kujumuika nanyi katika siku hii muhimu sana katika kuenzi mchango wa mgunduzi wa maandishi ya Braille ambayo yameleta ukombozi mkubwa wa maisha ya wasioona ulimwenguni kote. Wizara yangu inapenda kuipongeza Taasisi ya Huduma na Maendeleo kwa Wasioona Tanzania (TNIB) pamoja na wadau wote wa masuala ya watu wasioona kwa kuamua kuiadhimisha siku hii hapa Tanzania kwa mara ya pili.
Nafahamu kuwa Mataifa mengine Duniani yamekuwa yakiadhimisha siku hii miaka mingi iliyopita, hata hivyo wahenga husema kuwa kawia ufike, hivyo na sisi tumekwishaungana na Mataifa hayo na tutaendelea kuienzi siku hii muhimu.

Ndugu Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kulipongeza Kanisa la Anglikan Tanzania kwa kuona umuhimu wa kuanzisha shule kwa ajili ya Wasioona. Aidha nayapongeza madhehebu mengine pamoja na Serikali kwa kufuata mfano huo, jambo ambalo limesaidia sana kubadili mtizamo hasi na potofu dhidi ya watu wasioona kuonekana kwamba hawana mchango wowote katika maendeleo ya Taifa na Jamii zao. Wasioona ni nguvu kazi ambayo haina budi kuendelezwa kwa faida yao na Taifa kwa ujumla. Serikali ya Tanzania iko tayari kushirikiana na kutoa msaada kwa Asasi mbalimbali zinazojihusisha na uboreshaji wa maisha ya watu wasioona nchini. Hii inathibitishwa na hatua ya Serikali ya kutengeneza Sera na Sheria maalum ya watu wenye ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010. Hatua hii itasaidia sana kuhakikisha kwamba haki za msingi za wasioona na watu wenye ulemavu kwa ujumla zinalindwa na kutekelezwa.
Serikali imeishatunga Kanuni za Sheria hiyo, hivyo ni kazi ya Serikali na Asasi zote za watu wenye ulemavu kuwaelimisha wadau wao kuifahamu sheria hii na kudai haki zao kisheria.

Ndugu Mwenyekiti, napenda niwapongeze sana Wasioona wote kwa kutumia fursa zinazotolewa na Serikali na Asasi za Kiraia katika kujiendeleza Kielimu na  Kiuchumi. Wasioona wengi wanavyo vipaji na uwezo katika nyanja mbalimbali ambavyo vikitumika vizuri Taifa linaweza kunufaika kwa vipaji vyao. Kwa kutumia sheria ya Watu wenye Ulemavu, Wizara yangu kwa kushirikiana na Wizara mbalimbali itaweka mikakati endelevu itakayowezesha watu wenye ulemavu kufurahia maisha yao kama raia wengine. Pia napenda niwahakikishie kuwa Baraza la watu wenye ulemavu litaundwa haraka iwezekanavyo pamoja na kuzindua mfuko maalum wa watu wenye ulemavu ambao utasaidia sana kuwezesha shughuli zenu kuendeshwa kwa uhakika.

Ndugu Mwenyekiti, nafahamu kua mko katika mchakato wa kuanzisha mradi wa Kiwanda kidogo cha kutengeneza fimbo nyeupe zinazotumiwa na Wasioona. Serikali kupitia Wizara yangu iko tayari kushirikiana nanyi kuhakikisha kwamba mradi huu unafanikiwa. Fimbo nyeupe imetambuliwa rasmi kisheria katika Sheria ya watu wenye Ulemavu, hivyo ni wajibu wa Wizara yangu kuona kwamba mpango huu unafanikiwa. Kwa kuunga mkono jitihada zenu napenda kutoa changamoto kwa watu binafsi, mashirika na Serikali kwa ujumla kuona umuhimu wa kuchangia mradi huu. 

Ndugu Mwenyekiti, kuhusu changamoto zinazowakabili katika upatikanaji wa vifaa na machapisho mbalimbali katika Breille, Wizara yangu itashirikiana na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Tamisemi kuzipunguza changamoto hizi. Ninawaomba wasioona wote hususani wenye umri wa kwenda shule wapelekwe shuleni na wale ambao umri wa kwenda shule umepita wapelekwe katika vyuo mbalimbali vya mafunzo ili kuwapatia stadi na ujuzi wa kuwawezesha kujitegemea. Pia napenda kutoa wito kwa wananchi wote kuhakikisha kwamba wanatunza Afya ya macho yao na wanapoona kuwa wanasumbuliwa na matatizo ya macho wasisite kwenda katika Hospitali zilizo karibu nao. Kwakufanya hivyo wataweza kubaini haraka na kuepusha athari zinazoweza kuwasababishia kutoona.

Ndugu Mwenyekiti, mwisho napenda niwapongeze sana kwa kuandaa maadhimisho haya na pia niwashukuru wadau mbalimbali waliochangia kwa hali na mali kufanikisha maadhimisho haya. Naahidi kuwa kuanzia maadhimisho yajayo Wizara yangu itaendelea kuchangia katika kufanikisha maadhimisho haya.
Napenda  niwashukuru tena kwa kunialika kuwa Mgeni rasmi katika maadhimisho ya mwaka huu. Nawatakieni mafanikio mema katika shughuli zenu na heri ya mwaka mpya 2013.

Asanteni sana kwa kuniskiliza.
Read More ->>
 

| DISABILITY IN TANZANIA INFORMATION PLATFORM © 2012. All Rights Reserved |Designed by MIRAMBO GROUP | Back To Top |